Kupata Passport ya kusafiria ya kawaida Tanzania ni mchakato wa takribani wiki mbili unakuwa umepata passport yako lakini inaweza kwenda hadi miezi miwili au mitatu kwasababu mbali mbali kama ilivyokuwa kwangu.
Iwe unataka kuwenda kutembea au unatafuta kitambulisho cha kimataifa ili kuhakiki akaunti zako (Verification), kufahamu hatua kwa hatua nini kinahitajika, mchakato wake ukoje mwanzo mwisho ni jambo la msingi sana.
Katika mwongozo huu, nitakueleza kila kitu unachopaswa kufahamu kwa sababu mimi mwenyewe nimefanya, kwa ufupi gharama ya serikali ya kuomba passsport ya kawaida ni Tsh 150,000/= ila wewe hakikisha una bajeti ya 200,000/=
Kwa nini niliamua kutafuta Passport?
Watu wengi huanza kutafuta passport wakiwa na safari tayari, lakini kwangu ilikuwa tofauti. Kitu kilichonisukuma zaidi ni hitaji la ku-verify akaunti yangu ya LinkedIn. Licha ya kuwa na kitambulisho cha NIDA, LinkedIn wanahitaji Passport pekee.
Hapo ndipo nilipoingia kwenye mchakato huu na kujifunza mengi ambayo nitakushirikisha hapa ili wewe usipate tabu niliyopata mimi.
Vitu 6 unavyotakiwa kuwa navyo kabla ya kuomba Passport
Haya ndiyo yaliyoniwezesha mimi kupata passport.
Cheti cha kuzaliwa cha kwako.
Namba ya NIDA
Cheti cha Kuzaliwa cha Mzazi mmoja wapo (Au Kiapo cha Uraia – Affidavit).
Mara nyingi wazazi wetu hawana vyeti vya kuzaliwa, cha kufanya hapo nenda kwa Mwanasheria yeyote atakuandikia hicho kiapo kinachoonyesha Mzazi wako ni Mtanzania. Hakikisha taarifa unazotoa ni za kweli.
Wanasheria wanajua watakuandikia vizuri. Kuhusu pesa mfano mimi Mwanasheria wangu aliniambia 20,000/= ambayo ni kawaida ikizidi hapo umepigwa (Makubaliano).
Ni vizuri pia uwe na copy ya kadi ya NIDA ya mmoja wa wazazi wako. Itoe copy utaiambatanisha baadae. Ni njema zaidi ikiwa ya mama.
Barua ya Utambulisho kutoka Serikali ya Mtaa.
Nenda serikali ya mtaa waambie wakupe form ya utambulisho, utaijaza au watakusaidia kuijaza na watakupatia.
Kuhusu pesa haizidi 4,000/= ikizidi umepigwa, wengine huwa ni bure inategemea unaisha sehemu ipi.
Passport size moja.
Kama hauna basi mwambie jirani yako au rafiki yako akupige ama uenda kwa wanaopiga Pasipoti utachagua mwenyewe kipi bora ila mimi nilipiga kwa simu yangu nika-crop biashara ikaishia hapo.
Hii passport utaitumia tu kwenye kufanya maombi online lakini itakayoonekana baada ya passport kutoka ni ile utakayopigwa siku ukienda uhamiaji.
Barua ya Maombi Binafsi (Inayoelezea sababu ya kusafiri)
Hii ni tofauti na barua kutoka serikali ya mtaa. Hii inatakiwa iwe fupi hata aya moja inatosha kama zile tulizokuwa tunaandika kipindi kile tuko form two.
Angalia mfano hapa
Hii ni lazima uiandike mwenyewe kwa kutumia laptop au uende stationary wakupige hela au unasemaje!.
NB: Hapa usidanganye ikiwa kweli unasafiri maana unaweza kukamatwa huko, kwenye maombi umeandika unaenda kusoma/kutembea halafu ukakutwa unafanya biashara aisee mimi simo kwenye hiyo kesi yako.
Pale Uhamiaji utaulizwa pia endapo majibu yako yatakinzana na kile ulichokiandika kwenye Barua, Utarudishwa.
Hivi ndio vitu pekee vilivyoniwezesha mimi kupata passport. Bila hivi utakuwa bado hujatimiza vigezo vya kufanya maombi ya Passport Uhamiaji.
Hatua kwa hatua jinsi ya kuomba passport kwenye mfumo wa Uhamiaji Tanzania
Hii ni hatua ya kwanza ambayo unatakiwa uifanye ukiwa popote. Usiende ofisi za uhamiaji mfano pale ofisi za uhamiaji kurasini, Dar es Salaam kabla haujamaliza maombi ya awali kwenye mfumo.
Kama huniamini jifanye kama hujasoma hii uende utanikumbuka baadae.
Ni vizuri utumie laptop au Desktop ukiwa unafanya maombi online maana kwenye simu itakusumbua bure.
Bonyeza hii link Apply passport itakupeleka kwenye website ya uhamiaji tayari kwa kuanza maombi. Kama hujajisajiri jisajiri na kama tayari basi utaweka namba ya simu na kumbumbuku namba yako.
Hapa naomba tuelewane kumbukumba namba utakayopewa hakikisha unainakiri sehemu maana utaulizwa karibia kila sehemu utakayoenda hata kwenye mfumo wa uhamiaji uki log out itakuomba hiyo kumbumbuku namba. Ukiisahau umeisha narudia ukiisahau umeisha.
Vipengele Muhimu kuvifahamu ukiwa unajaza taarifa zako
Jaza kila sehemu taarifa sahihi kwenye hiyo form. Vitu vichache ambavyo utakutana navyo na huenda usivielewe ni hivi vifuatavyo.
Namba ya Uraia – hii ni namba ya NIDA
Kazi
Hapa andika cheo chako. Hakikisha una ushahidi usibuni cheo maana kule uhamiaji ukienda wanaweza kukuomba ushahidi.
Mfano mimi niliandika Freelancer kwako wewe weka cheo chako. Hakikisha tu unachoandika ndio kazi yako na unaweza kujitetea.
Jaza na upload vitu vinavyohitaji sehemu husika kama nilivyokuelekeza hapo juu hadi utakapofika sehemu ya malipo. Watakupa CONTROL number ulipie, lipia 20,000/= tu.
Ukilipia itafunguka hiyo hatua ya mwisho. Utadownload hiyo document nzima na utaenda kui print.
Tumemaliza hatua ya kwanza.
Hatua inayofuata ni kwenda ofisi za uhamiaji ukiwa na document zote zikiwa printed. Nisisahau, NIDA yako pia itoe copy na uiambatanishe.
Ukifika ofisini ulizia sehemu unaweza pata Muhuli wa mwanasheria hapo hapo uhamiaji utaonyeshwa na watakupangia document zako vizuri. Gharama ya muhuli ni 10,000 sidhani kama itazidi hapo ikizidi umepigwa.
Baadae utaziwasilisha hizo document zote zitakaguliwa kisha utapewa control number ulipie 130,000/= kwa passport ya kawaida.
Mpaka hapo utakuwa tayari umemaliza zoezi utakusanya hizo documents baadae utaitwa utaulizwa maswali ya hapa na pale, utaenda kupigwa picha na utaambiwa siku ya kwenda kuichukua na ni sehemu gani. Ni hivyo tu simple!
Hakikisha unawahi kwenye ofisi zao maana watu ni wengi saa moja kamili asubuhi uwe umefika.
Itachukua muda gani kupata kupata Passport yangu
Kitaalamu huwa inachuua siku 14 tu lakini kwangu ilikuwa tofauti imenichukua miezi mitatu kuipata. Tarehe ambayo niliambiwa nikaichukue pale Wizara ya Mambo ya ndani nilikuta bado haijatoka nikapigwa kalenda.
Kwako wewe ukiambiwa ukachukue tarehe fulani halafu hiyo siku ukaenda na ukaambiwa haijatoka hapo ongeza mwezi mmoja ndio uende tena vinginevyo utakuwa kama umeajiriwa pale.
Aidha ikiwa una uharaka wa kusafiri na ushahidi unao mfano tiketi ya ndege, barua ya ajira au masomo basi unaweza kuipeleka ofisi ya uhamiaji kuomba upatiwe Passport kwa uharaka. Hii itakuokoa kuliko kusubiri.
Kama utakuwa na nyongeza ama swali lolote uliza hapa hapa au nichek WhatsApp HAPA tupange ni nchi gani tuende mwaka huu.
Takribani wiki mbili zilizopita nilipigiwa simu na mfanya biashara mmoja akisema nimsaidie kutengeneza website. Website ambayo mtu akiitembelea awe convinced directly kuwa mteja wake, yeye yuko tayari kulipa kiasi cha pesa ilimradi tu hayo matokeo anayoyataka ayaone.
Nilijaribu kumwelekeza kuwa kwa upande wa website sisi tutafanya mikakati ya SEO kuifanya website yake ipande kwenye search engine ili mtu anapotafuta huduma unayoitoa aweze kukuona kirahisi kwenye search result ya google. Tutatoa mapendekezo maudhui yaweje kwenye website ili kuvutia zaidi.
Baada ya hapo mtu hawezi kushawishika moja kwa moja kununua huduma yako kwa kutembelea website yako tu kuna mambo mengi ambayo humfanya mteja afikie maamuzi ya kununua huduma yako ikiwemo maudhui yaliyopo kwenye website, muonekano wake lakini pia utofauti wako kwa social media (positioning).
Sababu kwenye website kuna sehemu ambayo huwa tunaweka social media links mtembeleaji aki-click hizo link je huko kwenye social media atakuona kama ulivyojionyesha kwenye website?
Je, marketing strategies zako zitamfanya mtu arudi tena kwenye website au ashawishike kununua bidhaa yako, brand yako ikoje?
Website pekee haiwezi kukufanya upate wateja mtandaoni bali itakujengea visibility shikamavu mtandaoni.
Gharama ya kutaka kuuza leo leo
Mfanya biashara anakupatia fedha kwa mashart kweli kweli: “Nataka ndani ya mwezi huu nianze kuona matokeo, nipate wateja wa kutosha, followers wengi, I want to see big numbers n.k.”
Ni kweli hakuna mtu ambaye anataka kutoa pesa yake halafu baadae asione matokeo. Hakuna. Kila mtu anataka kuona amepiga hatua kwenye kazi yake lakini ni vyema kujua ukweli kuhusu kupata wateja mtandaoni kabla hujaazimia kuanza kuuza bidhaa/huduma zako mtandaoni.
Inabidi ujue kuwa kuna mchakato hapa katikati mpaka kuwapata wanunuzi wa bidhaa yako ambao ni :
Brand awareness (Watu wakufahamu)
Build community (Watu wakuamini)
Conversion (Watu wahamasike kununua)
Wengi wanakosea hapa:
Anarusha matangazo kwa media either yeye mwenyewe au marketers aliowalipa, akitarajia kupokea utitiri wa wateja. Lakini, asilimia 80 ya simu zinazopigwa zinaishia kwa watu kuuliza maswali kisha wanachikichia mitini. Kweli, idadi ya followers inaongezeka, lakini cha ajabu, mauzo hayaongezeki.
Kwenye tangazo, comments zinasoma 1k hadi 5k lakini matokeo anayoyatarajia yanagonga mwamba kila kukicha. Mteja anaanza kuwalaumu marketers kwa kushindwa kufikia matarajio yake.
Ikiwa anapata yote hayo, shida ni nini hasa?
Shida kubwa ni kwamba mfanya biashara anataka kuuza leo leo kupitia tangazo au matangazo mawili matatu aliyoyatengeneza jambo ambalo ni gumu kulifanikisha, hajui umuhimu na kujenga msingi thabiti kwenye mitandao ya kijami ili apate matokeo anayoyahitaji.
Kuanza na malengo ya haraka bila kuwekeza katika brand awareness na kujenga community ni sawa na kujenga nyumba bila msingi imara.
Watu wengi wanaweza kuona bidhaa yako lakini kama hawakufahamu au hawana imani na brand yako, hawatachukua hatua ya kununua.
Matokeo hayo yanatokana na ukosefu wa uelewa kuhusu safari ya mteja (customer journey) na jinsi inavyohusiana na mauzo.
Kwanza, ni muhimu kuhakikisha kuwa watu wanakufahamu (awareness), kisha wanakutambua na kukuamini (community building) na mwisho wanakuwa tayari kununua (conversion). Hii ni safari inayohitaji muda, uvumilivu, na mikakati sahihi.
Maudhui unayotengeneza leo yanaweza kukupa wateja wengine miezi sita ijayo. Jaribu kuliangalia soko kwa miazi sita inayokuja utakuwa katika hali gani.
Ni muhimu kujua mchakato mzima wa masoko utakaoupitia na nini kinachohitajika ili kufikia malengo yako ya kuuza mtandaoni kwa urahisi.
Mwisho
Kabla ya kurusha matangazo, ni vyema kuanza kwa kuwekeza muda na fedha katika kujenga brand awareness na community.
Hii itahakikisha wanunuzi watakapokuwa tayari wamefahamu na kukuamini basi watakuwa tayari kuchukua hatua ya kununua bidhaa au huduma yako. Mkakati huu wa hatua kwa hatua utaongeza uwezekano wa kupata matokeo ya kudumu, badala ya matokeo ya haraka yasiyo na msingi.
Mafanikio ya kweli kwenye masoko ya kidigitali hayaji bin vuu kwa usiku mmoja. Inahitaji uvumilivu na uwekezaji wa muda mrefu. Post yako leo inaweza kukuletea mteja miezi miwili ijayo lakini ukitaka kuuza leo leo utajikuta unaungana na wale wanaosema “Mitandao haisaidii”
LinkedIn ni chuo kilichosheheni walimu waliobobea kwenye fields zao. Ukiachana na kupost, ukitulia vizuri na ukaamua kujifunza kutoka kwa watu wengine, kuna vitu vingi utajifunza tofauti na mtu ambaye hayupo kabisa LinkedIn.
Wapo watu ambao yamkini hawajapata fursa yoyote lakini kuwepo kwao linkedin wamehamasika kubadili maisha na mitazamo yao kwa ujumla.
Binafsi SEO, personal branding na mambo ya marketing nimejifunza kupitia LinkedIn learning. Kuwepo linkedIn kumenisaidia sana katika career yangu.
Tuangalie umuhimu wa wewe kuwepo LinkedIn katika kujifunza.
1. Linkedin ni jukwaa la kujifunza na kukua kitaaluma.
LinkedIn ni tofauti na majukwaa mengine yalivyo. Hili jukwaa siyo tu la kuchapisha habari au kutafuta kazi; ni mahali pa kujenga connection, kunoa ujuzi, na kupata maarifa mapya kila siku.
Kupitia posts zako watu watakupongeza na kukuchallenge kuhusu taaluma yako jambo ambalo ni zuri katika kujifunza. Hii itakufungua ubongo ubadili mtazamo juu ya hicho unachokijua sasa.
Ukiona posts zako zinapata negative comment usiwaze sana ni mambo ya kawaida mtandaoni.
Pia LinkedIn inakupa uwezo wa kushirikiana na watu wenye ujuzi wa hali ya juu kitaaluma kukuzidi kwenye sekta mbalimbali, na kwa kusoma makala zao zenye kuelimisha unaongeza madini mapya yatakayokusaidia kukuza taaluma unayojishughulisha nayo.
Cha kufanya chagua watu wako watano fuatilia makala zao kila siku, hudhuria event zao (virtual events), na shiriki kwenye posts zao hakika utaweza kufungua milango ya fursa nyingi ambazo huenda pengine usingezipata popote.
2. Kujiendeleza kiujuzi kupitia linkedIn learning
LinkedIn pia ina sehemu muhimu sana inayoitwa LinkedIn Learning. Hiki ndicho kitu muhimu sana kwa kujifunza na ndiyo kitu kilinifanya niazimie kusema linkedin ni chuo. Iwe wewe ni mfanyabiashara, mhitimu, mfanyakazi au CEO, hii ni sehemu sawadata ya kujifunza maarifa mengi zaidi.
LinkedIn Learning ni jukwaa la mtandaoni lenye maelfu ya kozi zinazotolewa na wataalamu kutoka sehemu mbalimbali duniani. Uzuri wake ni kwamba kozi hizi zote zinatolewa bure kwa mwezi mmoja wa mwanzo. Jifunze jinsi ya kujiunga LinkedIn premium bure leo hii upate kufaidika na kozi zilizopo.
Kupitia LinkedIn Learning, unaweza kujifunza kila kitu kutoka kwenye masuala ya teknolojia, biashara, uongozi, hadi kwenye ujuzi wa mawasiliano na usimamizi wa miradi. Faida kubwa ya kutumia LinkedIn Learning ni kwamba unaweza kujifunza kwa kasi yako mwenyewe, popote ulipo, na muda wowote.
3. Inakupa uhuru wa muda wa kujifunza.
Hii inamaanisha hata kama una ratiba ngumu, bado unaweza kupata muda wa kuongeza maarifa na ujuzi mpya ambao utakuongezea thamani katika soko la ajira. Moja ya vitu vya kipekee kuhusu LinkedIn Learning ni kwamba kozi zake zimeundwa kwa namna ya kiutendaji.
Badala ya kupata nadharia tu kama ilivyo chuoni, hapa unapata pia maarifa ya jinsi ya kutumia ujuzi huo katika maisha halisi ya kazi ofisini kwako.
Hii inakusaidia si tu kujifunza bali pia kuwa na ujuzi unaohitajika kwenye nafasi yako ya kazi. Kwa mfano, kama unataka kuboresha ujuzi wako wa uongozi, unaweza kuchagua kozi zinazohusiana na uongozi na usimamizi, kisha ukajifunza mbinu mbalimbali zinazotumika kwenye mazingira yako ya kikazi.
4. LinkedIn learning inatoa cheti kwa kila course.
Ukimaliza chuo unapewa cheti (Certificate) the same na linkedin unapomaliza kozi yoyote LinkedIn Learning unapewa cheti ambacho unaweza kuweka kwenye profile yako LinkedIn. Vyeti hivi vinaweza kuwa na uzito mkubwa, hasa unapojitambulisha kama mtu anayejali maendeleo ya kitaaluma na anayeendelea kujifunza kila mara.
Mfano ukiangalia profile yangu ya LinkedIn sehemu ya Certification and Licence utakuta kuna vyeti nilivyovipata linkedIn Learning nimeviambatanisha pale. Kwako vyeti hivyo vitaongeza mvuto wako kwa waajiri au wateja watarajiwa.
Mwisho wa yote, LinkedIn Learning inathibitisha kwamba kujifunza hakuishii darasani pekee. Katika ulimwengu wa sasa wa kidigitali, ujuzi unapatikana popote, wakati wowote, na kupitia jukwaa kama LinkedIn, unaweza kufikia malengo yako ya kitaaluma na kuwa na mafanikio katika kazi na maisha yako kwa ujumla.
Kwa hiyo, ikiwa unatafuta jukwaa la kujifunza, kuboresha ujuzi wako, na kuongeza thamani yako katika soko la ajira, LinkedIn Learning ni rasilimali muhimu sana ya kuchukua hatua hiyo.
Changamoto kubwa inayosumbua vijana wengi ni tatizo la ajira. Kila sehemu utasikia ajira hakuna ila kazi zipo.
Umekuwa wimbo unaovunja rekodi kila siku kuanzia juu hadi ngazi ya familia.
Wimbo huu unaongoza kwa kuimbwa na wahitimu wengi wa vyuo hapa nchini na kuna wengine wamegeuza tatizo hili kuwa fursa. Jambo ambalo ni zuri.
Ukiwa chuo usikae tu kizembe jaribu kufanya mambo mbalimbali yatakayokusaidia kukwepa Unemployment baada ya kumaliza chuo. Ni bora kujiandaa mapema kuliko kusubiri hatima usiyoijua.
Kukabiliana na janga hili kuhusu mbinu gani utumie kutafuta kazi, kwanza inabidi ujiulize wewe kama mwanafunzi unataka kuwa nani? Mpaka sasa unafanya nini kuhakikisha unakuja kuwa huyo mtu?
Chukua kalamu na karatasi narudia chukua karamu na karatasi sasa hivi kaa pembeni peke yako anza kuandika what kind of a person do want you to be in 3 years to come? huwezi kufikiria sawa sawa upate majibu ya maswali haya kwa kusoma tu lazima uandike kwenye karatasi ndio unapata kutambua kwa ufasaha majibu ya maswali hayo.
Vijana wengi husema acha kwanza nimalize itajulikana mbele kwa mbele. Mbele ipi wakati ukimaliza chuo unaenda kwenu ambako kupata fedha ya vocha tu ni changamoto!
Hivi unafikiri ukimaliza chuo mambo yatanyooka kama unavyotarajia? hata wao walifikiri vivyo hivyo kilichotokea hawaamini hadi leo.
Haya hapa mambo matano (5) ya kufanya ukiwa chuoni
1. Chagua kitengo/somo moja utakaloteseka nalo hadi kumaliza chuo.
Ukiwa chuo huwezi kuwa vizuri kwa yale yote yanayofundishwa darasani na pengine usiyafanyie kazi kabisa maishani mwako japo ni vizuri kuyafahamu.
Ukiamua kusoma course fulani chagua kitengo kimoja tu utakachokuwa unasoma kila siku iwe mchana iwe usiku unakomaa nacho mpaka unamaliza chuo mfano ukiamua kuchakalika na network hakikisha network haikupigi chenga, pata taarifa zote zinazohusu network.
Kuanzia mwaka wa kwanza hadi mwaka wa mwisho unakomaa na network ama kwa hakika utakuwa vizuri sana baada ya kumaliza chuo kuliko yule anayehangaika na vyote leo yupo Business management kesho hacking kesho kutwa Software development. Wahenga walisema mtaka yote kwa pupa hukosa yote.
Komaa na kitu kimoja, hayo masomo mengine yasome kwa ajili ya kunawilisha cheti chako. Hapa naomba tuelewane kitu unachokisoma hakikisha unalijua soko lake vizuri siyo unakomaa na hiki mwisho wa siku unaishia kufanya vitu tofauti kabisa.
2. Anza kujitolea mapema.
Usisubiri mpaka umalize chuo ndio uanze kutafuta sehemu ya kujitolea. Chuo ndio sehemu nzuri ya kujitolea ikiwa bado unapata fedha ya kujikimu kuliko ile unamaliza chuo ndio unajitolea yaani hata ukipewa pesa kidogo inaishia kununua dagaa na usafiri.
Fanya ufanyavyo ili mradi upate sehemu uanze kujitolea, kipindi unamaliza chuo pengine waweza kuajiriwa kwenye hiyo hiyo taasisi au kampuni kwa kuwa utakuwa tayari unajua ABC kuhusu mambo yanavyofanyika.
Kuna majukwaa pia ya kidigitali ambayo unaweza kujitolea kwenye makampuni ya nje ikiwa bado uko chuo kama vile SkilledUp Life hapa utatengeneza profile yako na kuapply kazi kulingana na field yako.
Kipindi wenzako wanahangaika kutafuta kazi wewe utakuwa unahangaika kupanga mafaili. Ukijitolea mapema utapata uzoefu mapema utakaokusaidia baadae kujibu lile swali liuzwalo kwenye chumba cha usaili “una uzoefu wa miaka mingapi”.
3. Noa ujuzi wako kila siku.
Usitegemee tu kile unachofundishwa darasani. Mwanafunzi mzuri ni yule anayetaka kujua nyuma ya pazia pakoje.
Siku hizi kuna majukwaa mengi yatoayo kozi za bure na za kulipia mtandaoni ni wewe na bundle lako tu mfano YouTube hapa kuna kila aina ya kozi unayotaka kujifunza, kuna kila suluhu ya matatizo unayoyapitia.
Usiseme huna bundle mbona ukiingia Insta au Tiktok unamaliza masaa mawili na ushee kutizama short videos? Bundle unalo sema bado hujaamua kuwa serious hebu kuwa serious uone kama utakosa pesa ya bundle.
Kama unataka kupata kubali kupoteza. Hakuna kitu cha bure duniani lazima ulipie.
4. Ishi Maisha yako.
Chuo kuna changamoto moja. Kila kijana anataka aonekane yeye ndio yeye si mtoto wa mkulima si mtoto wa Waziri si mtoto wa mfugaji wote wanataka kuishi maisha sawa.
Mwingine akipiga simu nyumbani laki mbili kwake ni pesa ya chai wakati kwako ni pesa ya kula miezi miwili hapo unalipa na kodi kabisa.
Lakini ukiwa chuo unataka uishi maisha sawa na wao. Fanya ujikubali, usiishi maisha ya kuigiza kumbuka maisha siyo kuigiza, fuata kilichokupeleka chuo hao marafiki unaoshinda nao leo siku mkimaliza chuo kila mtu ataenda kwao na wewe utaenda kwenu.
Kama huamini subiri mmalize chuo. Ukimpigia mwenzako atakwambia yuko ofisini utampigia baadae wakati wewe upo huko ndani ndani kwenye shamba la ndizi – Itaba.
Kama serikali inakulipia ada na umebahatika kupewa pesa ya kujikimu (BOOM) itumie vizuri pengine inaweza kukusaidia huko mbeleni.
5. Chagua marafiki wa kuishi nao.
Bwana mmoja alisema nikitaka kukujua wewe ni nani na mwelekeo wako ni upi nionyeshe marafiki zako watano. Nikiwaangalia marafiki zako basi nitapat kukujua wewe ni nani.
Kama wanapenda mitoko na wewe utakuwa nusu yake, kama wanapenda kusoma na wewe ni nusu yake, kama wanafanya biashara na wewe ni nusu yake, kama wanapenda kucheza PS na wewe ni nusu yake.
Hebu angalia marafiki ulionao kwa sasa na mambo wanayoyafanya halafu angalia na yako kama yanatofautiana sana.
Kuwa na marafiki ambao hawaendi njia unayotaka Kwenda ni sawa na kujichimbia shimo la kujilaumu baadae.
Bora ujiengue mapema na haimaanisha uachane nao kabisa. Hapana.
Jiweke kando na fanya mambo kivyako vyako mkikutana sehemu bongeni kama hakuna lililotokea huku ukiwa na moja kichwani. Ukitaka kujua zaidi kasome kile kitabu cha ATOMIC HABIT by James Clear utaelewa zaidi ninachokwambia hapa.
Hao jamaa zako usiwachukie wala kujiona wewe ndio mwamba wa Lusaka, maisha siyo hivyo ishi nao kwa akili mana hao rafiki zako ndio wanaweza kukuletea michongo mingi endapo utakuwa na ujuzi zaidi kuwazidi wao.
Maisha ni watu ishi nao vizuri.
Chuo ni daraja tu unapita tumia muda mwingi kuifikirie sana kesho kuliko leo yako. kwa mawasiliano nitafute WhatsApp bonyeza HAPA. Nimalize kwa kusema hakuna anayeijua kesho maisha yako yapo mikononi mwako.
Linkedin ni jukwaa lenye jumla ya watu wapatao zaidi ya bilion moja kutoka nchi zaidi ya 200 ulimwenguni. Mtandao huu unakua kwa kasi sana kutokana na fursa mbalimbali ambazo watu waliojiunga wanazipata hasa wanaotafuta kazi na wanaotangaza biashara zao.
Kuna faida gani za kutumia mtandao wa LinkedIn? Katika makala hii nimeelezea faida tano za kutumia mtandao wa LinkedIn mbali na kutafuta kazi kama ilivyozoeleka kwa wengi.
Kujifunza.
Watu wengi wanajiunga LinkedIn kwa lengo la kutafuta kazi tu hasa vijana wanaomaliza vyuo, jambo ambalo linafanya baadhi yao kuja na mabango ya “Hi everyone, I am looking for new role and would appreciate your support. Thank you in Advance for any connection” baada ya hapo haonekani tena.
LinkedIn ni jukwaa linalokuwezesha wewe kujifunza mambo mengi yamkini hata yale uliyokuwa huyajui kutoka kwa wataalamu tofauti tofauti mfano HR, Engineer, Writers, Consultants, Career coach, Doctors, Marketers n.k wote hawa wako LinkedIn.
Uzuri ni kwamba watu hawa hufundisha mambo kadha wa kadha ikiwemo mambo gani ufanye na yapi usifanye kulingana na tasnia zao.
Mfano huko LinkedIn HR wanafundisha jinsi ya kujibu maswali ya interview ambayo mara nyingi watahiniwa huulizwa wakiwa kwenye chumba cha mahojiano (Interview) kama vile “Unafikiri ni kwa nini wewe unafit kwenye hii kazi, tueleze wewe ni nani, tuulize swali kama una swali n.k”
Career Coach wanafundisha vitu ambavyo unatakiwa kujua kabla ya kwenda kwenye interview mfano “Jinsi ya kuelezea ujuzi wako, namna gani unaweza kuhama kutoka kitengo kimoja kwenda kitengo kingine bila kwenda kuongeza Masters wala kwenda kukisomea hicho kitu chuoni”.
Haya yote utajifunza huko huko LinkedIn, ni wewe na utayari wako wa kujifunza.
Kuongeza marafiki wapya.
Marafiki hawa wanaweza kuwa ni wataalamu wanaokuzidi kimaarifa na kiujuzi, mnaendana au unawazidi kwa lengo la kubadilishana mawazo chanya katika tasnia zenu na pengine kufanya kazi pamoja.
Mara nyingi urafiki huu waweza kukusaidia kutatua changamoto mbalimbali usizoweza iwe kwa kuongea nao kwenye simu, message, kusoma posts zao au kukutana nao sehemu ili kujadili zaidi baada ya kujuana.
Amini kwamba, milima haikutani lakini ninyi mnaweza kukutana katika namna ambao hukuitegemea, “aah! Kumbe ndo wewe sikutegemea kama tutakutana”. Leo mtakutana linkedIn kesho mtakutana Arusha live, uso kwa uso na huyo ndio anaweza kuwa mwenyeji wako.
Leo mnaweza kuchati na kushiriki kwenye mijadala yenu pale LinkedIn lakini kesho inawezekana mkafanya kazi kwenye ofisi moja.
Kukuza Jina.
Kama hujulikani kuanzia ngazi ya wilaya, mkoa, kitaifa basi LinkedIn inakupa fursa ya kujulikana siyo tu ngazi ya kitaifa bali ngazi za kimataifa. LinkedIn inakufungulia dunia kuwa unachotaka.
Huhitaji kukwea pipa mpaka marekani ili ujulikane unahitaji kuandaa maudhui yako yenye mvuto, yenye kutatua tatizo fulani, yenye kufundisha au yenye kuburudisha. Kwa kufanya hivi watu watapata kukujua wewe ni nani na unafanya nini.
Hivyo itakuwa rahisi kwako kupewa fursa za kazi kutokana na kile unachokiandika LinkedIn kwa sababu watu tayari watakuwa wanakujua. Hiyo ndiyo maana ya kukuza jina LinkedIn.
Watu hununua kwa watu wanaowajua. Vile watu hawaamini sana mitandao itakuchukua miezi hata mwaka mpaka watu waanze kukuamini na kukupa fursa au ufanye nao kazi. Kuza jina lako mtandaoni kwanza watu wakufaamu fursa za kazi zitakuja baadae.
Kuwa mvumilivu milango ya fursa haifungukagi kizembe. Tia juhudi na nia matokeo utayaona mwenyewe.
Kukuza uandishi wako.
Baada ya kumaliza mtihani wa mwisho chuoni suala la kuandika huishia papo hapo. Pengine uandishi kwako ni changamoto sana je, ni sehemu gani unaweza kufanya mazoezi ya kujiendeleza kuandika au kufanya uandishi wako uwe umenyooka, fasaha?
Ukiniuliza mimi nitakwambia ni linkedin, kwa nini? Kwa sababu inakupa nafasi kubwa ya kuandika maneno mengi kadri uwezavyo, kuna sehemu ya posts na newsletter ambapo unaweza kuandika na kukuza uandishi wako siyo kama ilivyo X (Twitter).
Wengi hushindwa kujitosa na kiingereza chao cha you know kisa wataonekana si wasomi sana au utasikia ni vigumu sana kukaa na kuandaa maudhui kwa kuandika, practice makes more perfect anza hivyo hivyo mwisho wa siku mambo yatakaa mkao. Mchicha nao ulianza kama ua, mdogo mdogo unajifunza itafika wakati wewe mwenyewe utaoni kama mchezo tu.
Lengo la kuandika muda mwingine siyo uonekane unajua sana, au wewe ni smart sana lengo ni kufanya watu waelewe kwa urahisi kile unachokiwasilisha. Watu hawataki mambo magumu magumu be direct proportional kwa unachokipost.
Ikumbukwe: Mipaka ya lugha yako mipaka ya ulimwengu wako. Kingereza ni lugha ya kimataifa, kibiashara hivyo kwa namna yoyote ile inabidi uijue.
Kutunza kumbukumbu.
Nadhani ulishawahi kuweka kumbukumbu zako kwenye diary, notebook au kwenye application mbali mbali pia hata LinkedIn yaweza kutumika kwa miradi hiyo. Ukiweka post yako kule itakaa milele mpaka utakapoamua kuifuta mwenyewe.
Muda wowote waweza kuirejea, kujikumbushia au kutunza mawazo yako kule iwe kwenye post yako au kwa kuacha comment kwenye post za watu wengine.
LinkedIn is a note taking app.
Mwisho, LinkedIn ni mtandao wenye faida kedekede hasa kwa mtu mmoja mmoja na kampuni kwa ujumla.
Usijifungie ghetoni au kukaa offline kisa hujapata kazi, ukiwa LinkedIn utajifunza mengi sana.